Seneta wa kaunti ya Kakamega Cleophas Malala ameachiliwa na mahakama ya Kakamega kwa dhamana ya shilingi milioni 2.5 baada ya kukanusha mashtaka yanayomkabili ya madai ya wizi wa mabavu, kumpiga afisa wa IEBC na kuharibu mali miongoni mwa zingine kwenye uchaguzi mdogo wa eneo bunge la Matungu
Seneta Malala pamoja na watu wengine saba walifikishwa mbele ya hakimu mkuu Dolphin Alego na kukanusha mashtaka tisa na kisha kwa ujumla kuachiliwa kwa dhamana ya shilingi milioni 14.Wanane hao wanadaiwa kuzua vurugu, kuharibu magari na kuwaibia wanasiasa wa chama cha ODM shilingi elfu 300 madai ambayo wamekanusha.
Wakili wa wanane hao Charles Malala aliiomba mahakama hiyo kuwaachilia kwa dhamana akisema wateja wake ni watu wanaojulikana na hawawezi kutoroka, ombi ambalo lilikubaliwa
Haya yakijiri, baadhi ya wakaazi wa kaunti ya Kakamega waliofika kufuatilia kesi hiyo wamekashifu maamuzi ya mahakama wakidai kuwa yamechochewa kisiasa