Maafisa wa polisi eneo la Cheptais eneobunge la Mlima Elgon wameanzisha uchunguzi kubaini chanzo cha kifo cha mwanamke mmoja mwenye umri wa makamo ambapo mwili wake ulipatikana ukiwa na majeraha shingoni nyumbani kwake mjini Cheptais.
Kamanda wa polisi kaunti ndogo ya Cheptais Mwita Marwa anasema mwendazake bi Sarah Kimarong mwenye umri wa miaka thelathini na tisa alipatikana na maafisa wa polisi kwenye kitanda chake katika nyumba ya kukodesha mjini Cheptais akiwa uchi na majeraha shingoni na mguuni usiku wa kuamkia jana baada ya kupashwa taarifa na nduguye George Kimarong.
Aidha Mwita amewarai wananchi kushirikiana kikamilifu na maafisa wa usalama kwa kutoa taarifa muhimu zitakazopelekea kukamatwa kwa wahusika wa mauaji hayo japo amedokeza kuwa tayari uchunguzi unaendelea kufwatia tukio hilo huku mwili wa mwendazake ukihifadhiwa katika hifadhi ya wafu ya hospitali ya rufaa ya Bungoma.
Story by Richard Milimu